Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Italia umeadhimisha miaka 62 ya Muungano kwa kufanya Mkutano Mkuu wa Watanzania wanaoishi maeneo mbalimbali nchini Italia (wanadiaspora). Mkutano huo ulifanyika katika mji wa Napoli, Mkoa wa Campania chini ya uenyekiti wa Mheshimiwa Mbarouk Nassor Mbarouk, Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Italia, na kuhudhuriwa na wanadiaspora takribani 100 pamoja na wafanyakazi wa Ubalozi.

Katika hotuba yake, Mheshimiwa Balozi alipata fursa ya kuzungumza na wanadiaspora kuhusu umuhimu wa Muungano na kueleza kwa kina faida mbalimbali zilizopatikana tangu kuanzishwa kwake. Vilevile, Mheshimwa Balozi alisisisitiza kuhusu kauli mbiu ya mwaka huu ambayo inaeleza umuhimu wa kudumisha amani, umoja na mshikamano miongoni mwa Watanzania kama msingi imara wa maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Balozi aliwahimiza wanadiaspora wote kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuiletea nchi maendeleo kwa kuitangaza vyema Tanzania, pamoja na kushiriki kikamilifu katika kutafuta na kutumia fursa za uwekezaji na biashara. Pia, aliwakumbusha umuhimu wa kuheshimu sheria, kanuni na taratibu za nchi wanayoishi, sambamba na kudumisha maadili mema ya Kitanzania.

Aidha, masuala mbalimbali yanayowahusu wanadispora yalijadiliwa, zikiwemo changamoto wanazokabiliana nazo. Mheshimiwa Balozi alitumia fursa hii kutoa majibu na ufafanuzi kuhusu changamoto hizo na kuahidi kuendelea kushirikiana na Watanzania hao kutafuta ufumbuzi. Mkutano uliazimia kuendelea kuimarisha mahusiano na ushirikiano baina ya wanadiaspora na Ubalozi.